Waziri wa Elimu mheshimiwa Mutula Kilonzo amejitokeza bayana kuwaunga mkono wanafunzi waliogoma wakidai wanalazimishwa kuvaa marinda marefu zaidi....Akasema kuwa hata sketi likiwa fupi halina shida kwani watoto si "watawa!"..........Kwa muktadha huo nikalitunga shairi "kuusifu" uamuzi huu wa kipekee!
WAZIRI AMEPITISHA
Kalamu na karatasi, n'andike hili kwa kasi,
Nimimine zangu hisi,niseme zangu tetesi,
Nimpongeze farisi,nimpe kongole sisisi,
Waziri ametangaza,marinda yapande juu.
Nimependezwa hakika, ni uamuzi mwafaka,
Rinda refu ni dhihaka,kwa nchi 'loimarika,
Minofu ikifichuka,ishara "tumechanuka"
Waziri amekubali, wana wakude marinda.
Rinda hadi aridhini,halifai aswilani,
Fedheha kubwa shuleni,waziri amebaini,
Rinda refu ni la nini, kuvaliwa darasani?
Waziri amepitisha,nani wewe kuipinga?
Kidete amesimama,jukwaani akasema,
Rinda refu si salama,ni bovu tena la zama,
Fupi linalo heshima,halitazua zahama,
Waziri amepitisha,watoto wavae mini.
Binti zetu si watawa,hawafai kuonewa,
Wana uhuru kwamuwa,wapewe hino satuwa,
Tuache kuwaumbuwa,kuwashikia shokowa,
Waziri amekubali, tuvae tunavyotaka.
Kenya imeendeleya, usasa kukumbatiya,
Haifai kubakiya,nyuma mithili mikiya,
Hata mini kivaliya,wana hawana hatiya,
Mutula amepitisha,sketi refu si njema.
Mutula nakupongeza,wana 'mewatelekeza,
Wazo lako lapendeza,wizara waendeleza,
Mambo unayageuza,uzidi kutuongoza,
Waziri amepitisha, rinda fupi ni halali.
Totauti siioni,darasa na danguroni,
Kama si uhayawani, basi nambie ni nini,
Kilichobaki ni nini,Mutula tuelezeni?
Waziri amepitisha, darasa liwe danguro!
Mwisho ninahitimisha,kololo nimedondosha,
Musere ninafungasha,uyumbe 'mewasilisha,
Mutula yuatamausha,wazazi 'megadhabisha,
Waziri amepitisha,wana wavae kihuni. SOLOMON OLE MUSERE,
Chuo kikuu cha Kenyatta,
NAIROBI.
21 Julai 2012
Saturday, 21 July 2012
MOLA NITAKUTUKUZA
Waama, yote aliyonitendea Mungu siwezi kuyahesahu moja kwa moja.Beti zifuatazo zinajaribu kutaja japo baadhi ya mema na makuu aliyonitendea Maulana.
MOLA NINAKUTUKUZA:
Ninapanda jukwaani,nimhimidi Manani,
Nyingi swifa za yakini,zinitokazo moyoni,
Ndiye wangu tumaini, kimbilio maishani,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Umenipa afya njema, mie sina hata homa,
Umenitunza Karima,muweza mwenye rekhema,
Umenepusha zahama, isinipate tuhuma,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Kisomo 'menijaliya, nasoma bila udhiya,
Karo wanigharamiya, kwa wema wako Jaliya,
Motisha 'menipa piya,nipate kuendeleya,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Kila siku twasikiya, ajali zimetokeya,
Roho zimeangamiya, na majuruhi mamiya,
Haya umenepushiya, kwa neemayo Jaliya,
Mola ninakutukuza,kwa yote lonitendea.
Vitendo vya kihalifu,nchini kwetu sufufu,
Maafa ni maradufu,kila kutwa yasadifu,
Pasipo wewe Raufu, mie ningekuwa mfu,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Nikupe nini muweza, hidaya ya kupendeza?
Nimejaribu kuwaza, kuipata sijaweza,
Wemawo wa kushangaza, popote nitangaza,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Daima humithiliki,Rabana msitahiki,
Ewe ndo wangu rafiki,kwenye faraja na dhiki,
Daima hunigeuki, Jalia mpenda haki,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Mikono na'kwinulia,kwako ninakimbilia,
Zaburi nita'kwimbia,kinywani mwangu Jalia,
Katu sitanyamazia, makuu 'lonitendea,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Rabana uhimidiwe, jinalo libarikiwe,
Kwa swifa ushangiliwe,kwa nderemo hata shangwe,
Magoti na upigiwe,kwa dua usujudiwe,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Ukingoni nimefika, shairi 'metamatika,
Namshukuru Rabuka, Muumba aloswifika,
Utulinde mtukuka, tupate kuneemeka,
Mola ninakutukuza, kwa yote lonitendea.
SOLOMON OLE MUSERE,
Chuo kikuu cha Kenyatta,
11 Julai 2012
KONGOLE WANASIASA
Kwa moyo wa kujituma, najitolea mhanga kama mhanga kuisifia dhima sheshe wanayotekeleza wanasiasa wetu hasa hao wanaowania urais kwenye uchaguzi ujao.Nani kama wao!
KONGOLE WANASIASA
Hewaa ndugu hewaa,lau kipungu napaa,
Nangia bila fadhaa,kwa beti ziso mawaa,
Tega lako lau paa,tuwaswifu mashujaa,
Kongole wanasiasa,mafundi wa kutongoa.
Mafundi wa kutongoa,wasemi waso na doa,
Kalima mwazishopoa,kokote mnapotua,
Ahadi chekwa mwatoa, nyingine za kushitua,
Kongole wanasiasa,farisi walobobea.
Farisi walobobea,waama nawaswifia,
Kofia nawavulia,si shere nawachezea,
Kokote mwatuchochea, fulani kumchukia,
Kongole wanasiasa,walumbi wenye busara.
Walumbi wenye busara,na bonge la mishahara,
Japo nchi ni fukara,dhima yenu bar'abara,
Uchumi umedorora,'meadimika ajira,
Kongole wanasiasa,wakenya twawathamini.
Wakenya twawathamini,'tawarejesha bungeni,
'Tawatetea debeni,wangwana waso kifani,
Japo twala mapipani,pasi kivazi milini,
Kongole wanasiasa,wajumbe wasitahiki.
Wajumbe wasitahiki, nani atawadhihaki?
'Metuondelea dhiki,japo 'meinajisi haki,
Matendo yenu afiki, na ndimi tamu ja uki,
Kongole wanasiasa,maneno yenu matamu.
Maneno yenu matamu, mithili ya zamzamu,
Farisi wa kushitumu,kwa tenzi za kuhujumu,
Wajumbe nawaheshimu,japo ndimi zenu sumu,
Kongole wanasiasa,kusema kweli mwayuwa.
Kusema kweli mwayuwa,ahadi kuzipomowa,
Jukwaani mkituwa,wakata tunachachawa,
Viuno 'twavinenguwa, tuisahau shakawa!
Kongole wanasiasa, kipaji bora mnacho.
Mnacho bora kipaji,namshukuru mpaji,
Nawavisheni mataji,nimalize utungaji,
Sinione mjuaji,nguchiro mkosoaji
Kongole wanasiasa, kwa bora wenu 'wongozi.
Kikomo ninakomile,uyumbe 'meupatile,
Ziada siandikile,'nisije fumwa mishale,
Virago nafungatile,mwituni nijitomile,
Kongole wanasiasa,kwa sheshe wenu wajibu.
SOLOMON OLE MUSERE,
Chuo kikuu cha Kenyatta,
NAIROBI.
17 Julai 2012.
Tuesday, 29 May 2012
NAMTAFUTA KIDOSHO
PENZI LA DHATI
Bisimillahi Rabuka, illahi Mola muweza,
Mwanao nalalamika, upweke menilemaza,
Jamani nahuzunika,nani tanituliza?
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Asiwe mwenye papara,ninachelea chiriku,
Kimwana wa hapa bara, mgeni nitamshuku,
Kidosho mwenye busara, asokuwa zumbukuku,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Ninamsaka tabibu, alo na mwingi mahaba,
Yangu roho aitibu, kwa mapenzi yaso haba,
Awe wa kwangu swahibu, upweke umenikaba,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Awe na bora umbile, na twabia adilifu,
Mtoto mwenye sumile,mwenye haiba faafu,
Nitalivaa penzile, shingoni lau mkufu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Nitamtwika jukumu, yangu roho kutuliza,
Ashike hino hatamu, rohoni kuniliwaza,
Maneno yake matamu,upweke kuifukiza,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Awe na mwingi heshima, kwa wadogo na wakubwa,
Kimwana mwenye hekima, asiyetokwa ubwabwa,
Alo tayari kwa dhima, kutenda yalo makubwa,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Atanituza Rabana, tunda la roho yangu,
Matoni nikimuona, yatanitoka matungu,
Hakika tutapendana, malaika ua langu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Kaditama wa tamati,kalamu ninailaza,
Wazo langu siliati,narudia kutangaza,
Khaherini mabenati, dhima hino mewatweza,
Namtafuta kidosho mwenye penzi la hakika.
Bisimillahi Rabuka, illahi Mola muweza,
Mwanao nalalamika, upweke menilemaza,
Jamani nahuzunika,nani tanituliza?
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Asiwe mwenye papara,ninachelea chiriku,
Kimwana wa hapa bara, mgeni nitamshuku,
Kidosho mwenye busara, asokuwa zumbukuku,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Ninamsaka tabibu, alo na mwingi mahaba,
Yangu roho aitibu, kwa mapenzi yaso haba,
Awe wa kwangu swahibu, upweke umenikaba,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Awe na bora umbile, na twabia adilifu,
Mtoto mwenye sumile,mwenye haiba faafu,
Nitalivaa penzile, shingoni lau mkufu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Nitamtwika jukumu, yangu roho kutuliza,
Ashike hino hatamu, rohoni kuniliwaza,
Maneno yake matamu,upweke kuifukiza,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Awe na mwingi heshima, kwa wadogo na wakubwa,
Kimwana mwenye hekima, asiyetokwa ubwabwa,
Alo tayari kwa dhima, kutenda yalo makubwa,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Atanituza Rabana, tunda la roho yangu,
Matoni nikimuona, yatanitoka matungu,
Hakika tutapendana, malaika ua langu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.
Kaditama wa tamati,kalamu ninailaza,
Wazo langu siliati,narudia kutangaza,
Khaherini mabenati, dhima hino mewatweza,
Namtafuta kidosho mwenye penzi la hakika.
SOLOMON OLE MUSERE
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
2011.
Friday, 11 May 2012
ULIYATAKA MWENYEWE
ULIYATAKA MWENYEWE,
Mrembo nakuswabahi,natumai u buheri,
Fursa hino naiwahi, kukuasa kishairi,
Nanena yalo sahihi,nikwambile pasi siri,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Kidosho nilikupenda,posa nikakuletile,
Nawe juu ukapanda,kuwa mie mchochole,
Nenda basi mwanakwenda, Musere nikakwambile
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Bwanyanye kakughilibu,ukawa windo rakhisi,
Ukalikumbatia dubu, kwa tamaa ya ukwasi,
Kirinda pasi aibu, kikakutoka kwa kasi,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Mhuni ukampa fursa, lako tunda kulimega,
Mkazamia anasa, mahaba yaliponoga,
Kila siku kawa misa, kokote mkijibwaga,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Dunia hutoiweza, nilikupa mausiya,
Matusi 'kanilekeza, kisema nakuchongeya,
Ukajigeuza pweza, makaa kujipaliya,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Hakika niliumiya,kimwana ulipozama,
Mengi nilokutendeya, ukaleta uhasama,
Kabidi kunyamaziya,kwa soni nikiinama,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Haikupita miezi, akakuponyoka Keni,
Likavuruga penzi, kitumbua mchangani,
Ukaachwa na matozi, na ndwele humo mwilini
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Katu huoni fedheha, eti wajileta kwangu?
'Sitaraji msamaha, hilo muuze Mungu,
Ulotenda ni karaha,yalinitia utungu,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Kikomo ninapotia, kidosho ushasikia,
Katu sitochelea,ukweli kukuambia,
Hilo kero fikiria, ndo ujumbe nakuatia,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
SOLOMON MUSERE, FEB 2012.
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
Mrembo nakuswabahi,natumai u buheri,
Fursa hino naiwahi, kukuasa kishairi,
Nanena yalo sahihi,nikwambile pasi siri,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Kidosho nilikupenda,posa nikakuletile,
Nawe juu ukapanda,kuwa mie mchochole,
Nenda basi mwanakwenda, Musere nikakwambile
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Bwanyanye kakughilibu,ukawa windo rakhisi,
Ukalikumbatia dubu, kwa tamaa ya ukwasi,
Kirinda pasi aibu, kikakutoka kwa kasi,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Mhuni ukampa fursa, lako tunda kulimega,
Mkazamia anasa, mahaba yaliponoga,
Kila siku kawa misa, kokote mkijibwaga,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Dunia hutoiweza, nilikupa mausiya,
Matusi 'kanilekeza, kisema nakuchongeya,
Ukajigeuza pweza, makaa kujipaliya,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Hakika niliumiya,kimwana ulipozama,
Mengi nilokutendeya, ukaleta uhasama,
Kabidi kunyamaziya,kwa soni nikiinama,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Haikupita miezi, akakuponyoka Keni,
Likavuruga penzi, kitumbua mchangani,
Ukaachwa na matozi, na ndwele humo mwilini
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Katu huoni fedheha, eti wajileta kwangu?
'Sitaraji msamaha, hilo muuze Mungu,
Ulotenda ni karaha,yalinitia utungu,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
Kikomo ninapotia, kidosho ushasikia,
Katu sitochelea,ukweli kukuambia,
Hilo kero fikiria, ndo ujumbe nakuatia,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?
SOLOMON MUSERE, FEB 2012.
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
Subscribe to:
Comments (Atom)