Tuesday, 29 May 2012

NAMTAFUTA KIDOSHO

PENZI LA DHATI

Bisimillahi  Rabuka,  illahi   Mola  muweza,
Mwanao nalalamika, upweke menilemaza,
Jamani  nahuzunika,nani tanituliza?
Namtafuta kidosho,  mwenye penzi la hakika.

Asiwe mwenye papara,ninachelea chiriku,
Kimwana wa hapa bara, mgeni nitamshuku,
Kidosho mwenye busara, asokuwa zumbukuku,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Ninamsaka tabibu, alo na mwingi mahaba,
Yangu roho aitibu, kwa mapenzi yaso haba,
Awe wa kwangu swahibu, upweke umenikaba,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Awe  na  bora umbile, na twabia adilifu,
Mtoto mwenye sumile,mwenye haiba faafu,
Nitalivaa penzile,  shingoni  lau mkufu,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Nitamtwika jukumu, yangu roho kutuliza,
Ashike  hino hatamu, rohoni kuniliwaza,
Maneno yake matamu,upweke kuifukiza,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Awe na mwingi heshima,  kwa wadogo na wakubwa,
Kimwana mwenye hekima, asiyetokwa ubwabwa,
Alo tayari kwa dhima, kutenda yalo makubwa,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Atanituza  Rabana, tunda la roho yangu,
Matoni nikimuona, yatanitoka matungu,
Hakika tutapendana, malaika ua langu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Kaditama wa tamati,kalamu ninailaza,
Wazo langu siliati,narudia kutangaza,
Khaherini mabenati, dhima hino mewatweza,
Namtafuta kidosho mwenye penzi la hakika.

SOLOMON OLE MUSERE
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
2011.

No comments:

Post a Comment