Waama, yote aliyonitendea Mungu siwezi kuyahesahu moja kwa moja.Beti zifuatazo zinajaribu kutaja japo baadhi ya mema na makuu aliyonitendea Maulana.
MOLA NINAKUTUKUZA:
Ninapanda jukwaani,nimhimidi Manani,
Nyingi swifa za yakini,zinitokazo moyoni,
Ndiye wangu tumaini, kimbilio maishani,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Umenipa afya njema, mie sina hata homa,
Umenitunza Karima,muweza mwenye rekhema,
Umenepusha zahama, isinipate tuhuma,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Kisomo 'menijaliya, nasoma bila udhiya,
Karo wanigharamiya, kwa wema wako Jaliya,
Motisha 'menipa piya,nipate kuendeleya,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Kila siku twasikiya, ajali zimetokeya,
Roho zimeangamiya, na majuruhi mamiya,
Haya umenepushiya, kwa neemayo Jaliya,
Mola ninakutukuza,kwa yote lonitendea.
Vitendo vya kihalifu,nchini kwetu sufufu,
Maafa ni maradufu,kila kutwa yasadifu,
Pasipo wewe Raufu, mie ningekuwa mfu,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Nikupe nini muweza, hidaya ya kupendeza?
Nimejaribu kuwaza, kuipata sijaweza,
Wemawo wa kushangaza, popote nitangaza,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Daima humithiliki,Rabana msitahiki,
Ewe ndo wangu rafiki,kwenye faraja na dhiki,
Daima hunigeuki, Jalia mpenda haki,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Mikono na'kwinulia,kwako ninakimbilia,
Zaburi nita'kwimbia,kinywani mwangu Jalia,
Katu sitanyamazia, makuu 'lonitendea,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Rabana uhimidiwe, jinalo libarikiwe,
Kwa swifa ushangiliwe,kwa nderemo hata shangwe,
Magoti na upigiwe,kwa dua usujudiwe,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.
Ukingoni nimefika, shairi 'metamatika,
Namshukuru Rabuka, Muumba aloswifika,
Utulinde mtukuka, tupate kuneemeka,
Mola ninakutukuza, kwa yote lonitendea.
SOLOMON OLE MUSERE,
Chuo kikuu cha Kenyatta,
11 Julai 2012
No comments:
Post a Comment